Nzega, Tabora
Halmashauri ya Wilaya ya Nzega imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya wanufaika wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini (TASAF), ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma za afya kwa uhakika.
Akizungumza wakati wa kuanza kwa zoezi hilo, Mratibu wa TASAF wa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega, Bi. Jovita Patrick, amesema jumla ya kaya 2,621 zenye wanufaika 10,614 kutoka kata mbalimbali za wilaya hiyo zitanufaika na mpango huo. Amesema lengo kuu la mpango huo ni kuwezesha kaya zenye uhitaji kupata huduma za matibabu bila vikwazo vya kifedha.
Kwa upande wake, Msimamizi wa Ofisi Ndogo ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Wilaya ya Nzega, Bw. Haji Mpeta, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya viongozi wa ngazi za kata na vijiji katika utambuzi na uthibitishaji wa kaya husika ili kuhakikisha walengwa wote wanafikiwa kwa wakati. Ameeleza kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuboresha na kusogeza huduma za afya karibu na wananchi.
Naye Diwani wa Kata ya Utwigu, Mhe. Christina Ikaji, amepongeza kuanza kwa zoezi hilo katika kata yake na kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki zoezi la uandikishaji na upokeaji wa kadi za bima ya afya. Aidha, ametoa shukrani kwa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuimarisha sekta ya afya nchini.
Baadhi ya wananchi walioshiriki katika zoezi hilo wameishukuru Serikali kwa kuwajali na kuwapatia fursa ya kupata huduma za afya kupitia mpango huo, wakieleza kuwa hatua hiyo itapunguza mzigo wa gharama za matibabu kwa familia zao.
Zoezi la usajili na ugawaji wa kadi limefanyika katika vijiji vya Mwambaha, Isalalo, Utwigu, Mwanhala na Iyombo, na linatarajiwa kuendelea kwa siku 10 katika kata zote za Halmashauri ya Wilaya ya Nzega ili kuhakikisha walengwa wote wanapatiwa huduma hiyo muhimu.
MATUKIO KATIKA PICHA








Halmashauri ya Wilaya ya Nzega (Kata ya Utwigu kijiji cha Mwambaha Lubisu )
Anuani ya Posta: S.L.P 4
Telephone: 026 2692349
Simu ya Kiganjani: 0765600994
Barua pepe: md@nzegadc.go.tz
Hati miliki Halmashauri ya Wilaya ya Nzega @ 2017. Haki zote zimehifadhiwa