Halmashauri ya Wilaya ya Nzega mkoani Tabora imepokea zana za kisasa za kilimo aina ya powertiller (trekta tembezi) kutoka Wizara ya Kilimo kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuimarisha kilimo cha kisasa na kuongeza uzalishaji wa mazao nchini.
Powertiller hizo zimegawiwa katika skimu za umwagiliaji zilizopo kwenye kata sita za Wilaya ya Nzega ambazo ni Sigili, Nata, Kamanhalanga, Budushi, Lusu na Ikindwa. Ugawaji huo unalenga kuwawezesha wakulima kutumia teknolojia ya kisasa katika shughuli za kilimo, kuongeza tija, kupunguza gharama za uzalishaji na kuondoa utegemezi wa zana duni za kilimo.
Akizungumza wakati wa hafla ya ugawaji wa zana hizo, Mkuu wa Wilaya ya Nzega Naitapwaki Tukai amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kupitia Wizara ya Kilimo, kwa kuendelea kuwasogezea wakulima zana muhimu za uzalishaji. Aidha, amewahimiza wanufaika wa powertiller hizo kuzitunza ipasavyo na kuhakikisha zinawanufaisha wakulima wengi zaidi katika maeneo ya skimu za umwagiliaji.
Kwa upande wake, Mkuu wa Sehemu ya Kilimo Mazao katika Halmashauri ya Wilaya ya Nzega, Said Shemahonge, amewataka wakulima kuzingatia matumizi sahihi ya powertiller hizo kwa kufuata miongozo ya kitaalamu, ikiwemo kuepuka kuzitumia kubeba mizigo inayozidi uwezo wake, ili ziweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa muda mrefu.
Naye mmoja wa wakulima walionufaika na mpango huo ameishukuru Serikali na Halmashauri ya Wilaya ya Nzega, akieleza kuwa upatikanaji wa powertiller hizo utachochea ongezeko la uzalishaji wa mazao na kuboresha maisha ya wakulima.
Ugawaji wa powertiller hizo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha kilimo cha umwagiliaji, kuongeza uzalishaji wa mazao, kuhakikisha usalama wa chakula na kuinua kipato cha wakulima nchini.








Halmashauri ya Wilaya ya Nzega (Kata ya Utwigu kijiji cha Mwambaha Lubisu )
Anuani ya Posta: S.L.P 4
Telephone: 026 2692349
Simu ya Kiganjani: 0765600994
Barua pepe: md@nzegadc.go.tz
Hati miliki Halmashauri ya Wilaya ya Nzega @ 2017. Haki zote zimehifadhiwa